
Umekuwa ukimtumia jumbe (sms) msichana, umetumia emojis, memes, umefikiria jina zuri la utani (a.k.a) kwa ajili yake lakini bado hujaambulia jibu katika yote uliyoyafanya.
Unaweza ukawa umekaa unatafakari ni kitu gani ulichokosea kilichosababisha mrembo huyo asikujibu. Unawaza ni namna gani utaweza kukabiliana na hali hii kwani kila simu yako ikiita, unatamani awe ni yeye, kumbe wakati mwingine ni sms za kukumbushwa kwenda kusajili laini kwa alama ya vidole.
Kuna njia mbalimbali za kukabiliana na hali hii, lakini kabla hatujajadili hilo, embu jiulize swali moja, kwanini hajibu sms zangu?
Pengine ametingwa na shughuli zake, au ni mtu ambaye hapendi kutuma sms/hapendi kuchat sana. Lakini hapana, kutuma sms kunachukua sekunde chache sana, kiasi kwamba hakuwezi kumuharibia lolote kwenye ratiba yake.
Sasa je, kama hajibu unafanyaje?
Weka umbali kidogo
Kama msichana hakujibu sms zako, suluhisho sio kumbambikizia lundo la sms, kwa sababu kama hakujibu ujumbe mmoja, usidhani kuwa ukimtumia jumbe 100 basi ndio atajibu, zaidi atakublock, sababu ataona usumbufu.
Kubwa unalotakiwa kufanya hapa ni kupunguza mawasiliano, piga hatua moja nyuma, jioneshe kwa haujali. Fahamu kuwa, matunda yakiwa mengi sokoni, bei hushuka, lakini yakiwa machache bei huwa juu, hivyo lengo hapa ni kupandisha bei yako, hivyo usijioneshe sana, kuwa kila mara upo.
Upungufu utatengeneza uhitaji mkubwa.,
…Usiweke umbali mkubwa sana
Tulichojadili hapo juu haimaanishi kwamba ndio umsahau, hapana, mawasiliano lazima yawepo. Usiache zipite siku 2 au 3 bila kumtumia ujumbe japp mmoja.
Lazima uhakikisha suala la muendelezo (consistency) linakuwepo, maana ni moja ya vitu ambavyo wasichana/wanawake wanapenda sana. Haijalishi kuwa utakuwa unaandika nini kwenye ujumbe wako (ila isiwe tusi) lakini kwa vile kila mara utakuwa unamtumia, hilo linatosha.
Usiulize kwanini hajibu sms zako
Sheria ya msingi, usimuulize kwanini jana au juzi au wakati fulani nilikutumia ujumbe huu na huu lakini hukunijibu. Ukimuuliza itamuonesha kuwa yeye kuto kukujibu kulikuumiza au kulikusononesha. Lengo hapa ni kuonekana mkakamavu, na kwamba yeye kutokukujibu hakukusumbua kabisa.
Mfano ukimtumia ujumbe kumuuliza anafanya nini, lakini hakukujibu, baadae akaleta mada nyingine, usimkumbushe ule ujumbe ambao hakuujibu.
Kamwe usifanye japo kwa utani kumuuliza kuhusu yeye kutokukujibu, kama hakujibu, acha ipite, kikubwa uhai.
Chagua mada mpya ya mazungumzo
Ukimtumia ujumbe leo, asipokujibu, utakapokuja kumtumia tena kesho, usimtumie kuhusu jambo lile lile ulilotuma jana, chagua suala jingine la kuzungumzia, kwani huenda hakukujibu kutokana na ulichokizungumzia.
Pia unatakiwa kuonekana mpya, mwenye mawazo mapya na chanya kila siku. Mbali na kutaka akijibu, lengo jingine ni kumfanya atake au avutiwe kuonana na wewe.
Pia usisahau maswali ya kiuchukozi ambayo yataweza kumfanya atabasamu, mfano, unadhani wewe ungekuwa lugha, ungependelea kuwa lugha gani? Ni swali la kawaida, lakini litamfurahisha na kumfikirisha kabla hajakubu.
Zungumzia mambo chanya
Tumejikita zaidi kwenye kujadil nini usifanye, au nini usiseme. Lakini je? Vipi kuhusu nini cha kusema/kufanya?
Ibua mambo yenye majibu chanya, tumia emojis, memes kwenye simu yako kumshawishi akujibu. Pia usisahau jumbe zenye kumfurahisha. Unatakiwa kujua namna ya kumfanya msichana afurahi kwa kusoma tu ujumbe wako, hadi aanze kutafakari hutu mtu nikiwa nae ana kwa ana itakuwaje kama kwenye simu tu ananifanya nijisikie vizuri hivi.
Lengo ni kutengeneza mazingira ya urafiki wa juu juu kwanza ili akujibu au/na akubali muonane hata kama ataamua kukataa utakachomwambia.
Wasiliana na wasichana wengine
Ili kuweza kumuonesha kuwa hujali sana asipokujibu, lakini pia kukuwezesha na wewe kumsahau kwa baadhi ya nyakati, wasiliana na wasichana wengine ambao watakusaidi usiwe unamuwaza yule unayetaka akujibu.
Huweza ukaumizwa na msichana mmoja kutokukujibu wakati tayari unao wengine watano wanaokujibu na maisha yako yanakwenda.
Wale ambao huenda baa au kwenye kumbi za burudani wanaifahamu hii kanuni. Ili kumpata msichana unayemtaka, huwa wanazungumza na wasichana wengine wengi kwa makusudi ili mlengwa aone wivu, ahisi kwamba akichelewa itakula upande wa dereva.
Endapo baada ya jitihada zote hizi hatokujibu, tambua kwamba kikubwa ni uhai, na kuna jema hata katika mambo mabaya
